Showing posts with label news. Show all posts
Showing posts with label news. Show all posts

Tuesday, September 24, 2013

Samantha Lewthwaite: Gaidi anayedaiwa kuilipua Kenya


Taifa la Kenya, limekumbwa na tukio ambalo haliwezi kusahaulika masikioni mwa watu ambao ni wapenda amani. Tunavyosema hivyo, tunaamini kila mmoja anaelewa vizuri tukio la watu wanaosadikiwa kuwa magaidi, ambao waliteka jengo la Westgate mjini Nairobi na kusababisha vifo vya watu 69, huku 175 wakijeruhiwa vibaya.

Lakini katika tukio hilo, kuna mwanamke mmoja raia wa Uingereza mama wa watoto watatu, anadaiwa kuwa ni mmoja wa magaidi walioshiriki katika tukio hilo.

Mwanamke huyo mwenye itikadi kali, Samantha Lewthwaite, anajulikana kama ‘Mzungu Mjane’, ni mwanachama muhimu wa kundi la wanamgambo wa Kiislamu Al-Shabaab la nchini Somalia, ambalo limedai kuhusika na shambulio hilo.

Mwanamke huyo, ambaye amewahi kuwa askari wa Uingereza kutoka eneo la Aylesbury, Bucks, alisilimu dini kuwa Muislamu ambaye mumewe alikuwa mmoja wa watu waliojitoa mhanga wakati wa mashambulizi ya Julai 7,2005 mjini London.

Vyanzo vya habari, vilisema mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 29, huenda ni miongoni mwa wanamgambo hao walioficha sura zao ambao hadi tunaingia mitamboni jana jioni, walikuwa wamejichimbia katika kituo hicho cha biashara.

Picha za mitandao ya kijamii zilionyesha mwanamke huyo akiwa ameshikilia bunduki.

Katika ujumbe wa Twitter, kundi la Al-Shabaab lilimsifu mama huyo maarufu ‘Mzungu Mjane’ na lilijigamba kwamba liko pamoja nao.

Katika akaunti yao ambayo imekuwa ikifungwa mara kwa mara, waliandika: “Sherafiyah Lewthwaite aka Samantha ni mwanamke shupavu,tuna furaha kuwa naye!”

Umwagaji damu huo umeua watu 69 na 175 wakiwa wamejeruhiwa vibaya,wakiwamo watoto wenye umri hadi miaka miwili.

Ilianza saa 7 mchana Jumamosi, wakati wanamgambo wanaofikia 15 wakiwa na silaha nzito walipovamia jengo hilo la maduka ya kifahari lililopo kaskazini magharibi mwa Jiji la Nairobi na kurusha magruneti na risasi kiholela, huku wakiimba nyimbo za jihad.

Msemaji wa Ikulu ya Marekani, Manoah Esipisu alithibitisha ripoti kuwa mwanamke mzungu alikuwa miongoni mwa wanamgambo hao.

Chanzo cha habari cha polisi nchini Kenya kilisema: “Samantha Lewthwaite ni shabaha namba moja.”

Wakati maofisa wa usalama wakijiandaa kuanza shambulio la mwisho usiku wa kuamkia jana, katika jaribio la kuhitimisha umwagaji damu, maofisa wa Serikali walifichua kuwa wanamgambo hao walikuwa wakishikilia mateka takribani 30.

Chanzo kimoja kiandamizi kilisema: “Kuna uwezekano mkubwa Samantha Lewthwaite akawa mmoja wa magaidi. Tuna ripoti za kuwepo mwanamke mmoja au ikiwezekana wawili wanahusika na shambulio hili.”

Kiliongeza: “Kuna ishara kubwa, Lewthwaite ana uwezo na ushawishi ndani ya Al-Shabaab kuendesha unyama kama huo.”

Lewthwaite, ambaye mumewe mwenye itikadi kali ya Kiislamu, Jermaine Lindsay, alijilipua katika njia ya treni ya Piccadilly mjini London Julai 7, 2005, pia anasakwa kwa njama za ulipuaji bomu ambalo liliua mamia ya watalii wa Uingereza mjini Mombasa.

Pamoja na Mwingereza mwenzake, Jermaine Grant wawili hao walikuwa wamebakiwa na siku chache tu waendeshe shambulio lao kabla ya kukamatwa Desemba, 2011.

Grant kutoka London Mashariki, alitarajia kupanda kizimbani mjini Mombasa jana.

Alikamatwa kabla ya mpango wao hatari kufanikiwa, lakini Lewthwaite alifanikiwa kutoroka tangu hapo.

Hivi karibuni aliandika katika blogu yake: “Hofu inaweza kukufanya ufanye vitu vingi.”

Lewthwaite pia amehusika kutoa mafunzo kwa washambuliaji wa kike wa kujitoa mhanga katika nchi jirani ya Somalia.

Ilikuwa safari ya kutisha kwa mwanamke huyo aliyezaliwa kama msichana wa kawaida huko Aylesbury, kabla ya kukutana na Lindsay, ambapo wawili hao walioana miaka mitatu baada ya kukutana.

Wakati mumewe alipotajwa kuwa mmoja wa watu wanane waliojitoa mhanga katika njia za ardhini na kuua watu 52 mwaka 2005, Lewthwaite awali alilaani shambulio lililofanywa na mumewe na alikana kuhusika au kujua mpango wa mumewe.

Kumbe huo uliokuwa uongo mtupu, kwani miaka minane baadaye, Lewthwaite akatokea kuwa mmoja wa watafutaji wakuu wa wapiganaji kwa ajili ya mtandao wa Al Qaeda kwa ukanda wa Afrika Mashariki na msemaji rasmi wa Al Shabaab.

Pamoja na kuyalenga mataifa ya magharibi, Lewthwaite aliwahi kutumia mtandao wa Twitter kulaani makundi mengine hasimu ya kigaidi.

Hasira zake dhidi ya makundi hayo, zilijionesha kwa kifo cha Omar Shafik Hammami, mwanafunzi wa zamani kutoka Alabama. Wiki iliyopita alipigwa risasi na kufa katika shambulio la kushtukiza na magaidi wanaomtii ‘Mzungu Mjane. ‘Kifo chake na kiwe fundisho kwa wale wanaotaka kufuata nyayo zake,’ Lewthwaite aliandika katika mtandao wa Twitter.

Hata hivyo, hakueleza kuhusu mwanaume wa Uingereza anayeelezwa kuwa mumewe wa pili aliyeripotiwa katika shambulio hilo la kushtukiza nchini Somalia, baada ya kundi la Al-Shabaab kuingia mzozo wa uongozi.

Sifa yake ya kutoogopa kitu barani Afrika ambako mitandao ya kigaidi inazidi kukua, inaimarishwa na kuhusika kwake kama mujahid au shujaa, wakati wa mlolongo wa mashambulizi na ulipuaji mabomu katika maeneo ya kitalii.

Akijulikana na wafuasi wake kama Dada Mzungu, Lewthwaite alihamia Kenya akiwa na watoto wake watatu mwaka 2007.

Akiwa na umbo dogo na fupi, alikatisha uhusiano na familia yake nchini Uingereza na kuzamia kwenye mitandao ya kigaidi Afrika Mashariki, akiunganisha nguvu na Waingereza wenye itikadi kali ambao waliingia Kenya kuendesha vita ya ‘jihad’ dhidi ya wasio Waislamu. Ilikuwa mwaka jana maisha mapya ya siri ya Lewthwaite yakaibuka.

‘Mwanamke mzungu’, aliyetambulika kama Lewthwaite, aliongoza kundi la magaidi kurusha maguruneti katika baa mjini Mombasa, ukanda wa pwani wa kitalii maarufu kwa watalii wa Uingererza.

Watu watatu, akiwamo mtoto waliouawa na wengine zaidi ya 50 kujeruhiwa.

Haikuchukua muda akawa katika rada za maofisa wa usalama wa Kenya,lakini aliweza kuwakwepa kwa kuvalia mavazi ya Kiislamu akifunika uso na mwili mzima akitembelea kati ya Somalia, Kenya na Tanzania.

Saa 51 za mapambano


Westgate, zimeshuhudia jana milio mizito ya risasi na mabomu kutoka ndani ya jengo hilo. Mapambano kati ya askari wa vikosi vya ulinzi na usalama vya Kenya, yalipamba moto jana mchana na kusababisha moshi mzito kutoka ndani ya jengo hilo.

Tukio hilo lilitokea baada ya askari wa kikosi maalumu cha Kenya, wakisaidiwa na maofisa usalama kutoka nchi za Israel, Marekani na Uingereza, kuanza kazi ya kuwafikia wanamgambo wa Kiislamu wa Al-Shabaab. Waziri wa Mambo ya Ndani, Joseph Ole Lenku, alisema katika mapambano hayo, magaidi wawili waliuawa na mateka kadhaa waliokolewa.

“Wanamgambo wote ni wanaume, japokuwa baadhi walivalia kama wanawake.

“Tunadhani operesheni itafikia mwisho muda si mrefu,” alisema. “Tunadhibiti sakafu zote, magaidi wanakimbia na kujificha katika baadhi ya maduka. Hakuna sehemu ya kutorokea,” alisema Waziri Lenku.

Alisema kuna hofu idadi ya vifo huenda ikaongezeka, wakati askari wakiendelea kutafuta watu walionusurika na miili katika maeneo mbalimbali ya maduka.

Alisema karibu mateka wote wameokolewa kutoka jengo hilo, saa chache bada ya kukumbwa na mlolongo wa mashambulizi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Jeshi la Polisi, David Kimaiyo, alisema katika ujumbe wake wa Twitter kuwa katika siku ya tatu ya shambulio hilo, waliwaokoa mateka baada ya kuingia jengoni huku wakizidi kupata mafanikio dhidi ya washambuliaji.

Alisema jana mchana, kuna watu kadhaa waliokamatwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Nairobi, wakijaribu kutoroka.

Monday, September 23, 2013

Kweli ni kilele cha mapenzi?


Uvimbe mweusi unaoonyesha kuvilia kwa damu ulikuwa karibu na jicho lake, chini kidogo ya jicho la mkono wa kushoto, hali hii ilionyesha kuwa alipatwa na dhoruba fulani, na rangi yake ya 'mkorogo' ilizidisha athari kwenye uvimbe ule na kuonyesha hali ya 'hatari'.

"Vipi, imekuwaje?", alimuuliza rafiki yake ambaye ndiye niliyekuwa naye.

"Mwenzangu we acha tu!", alisema yule mwanamke mwenye 'ngeu' na kuongeza; "hawa wanaume wengine watatuua".
"Usiniambie kuwa shemeji kakupiga tena", akadadisi yule mwenzake ambaye sasa sauti yake iliyojaa huruma ilikuwa na shauku ya kujua kwa uhakika ni nini kimepata mwenzake.
"Ndio huyo huyo," akajibu yule mwanamke.

Kilichofuata ni hadithi ndefu ya kisa cha kipigo alichopata mwanamke yule, alieleza kuwa mpenzi wake alimpiga baada ya yeye kuacha kupokea simu yake na alipoenda nyumbani kwake hakumkuta, na kwa maneno ya mwanamke huyo ni kwamba siku hiyo alikuwa na mashoga zake kwenye dansi la bendi moja maarufu.

Kwa 'hesabu' za harakaharaka, mtu anaweza kusema kuwa mpenzi wa mwanamke huyu hakuwa na sababu za kumpiga na kumuumiza mpenzi wake kiasi hicho, kwenda dansi na mashoga zake tu iwe sababu ya kumpiga kiasi hicho?
Lakini, 'ukipiga hesabu' nyingine, utaona kuwa mwanamke yule naye alikuwa na kosa, iweje aende dansini bila ya kumuaga mpenzi wake? Na kwa nini pia asipokee simu yake wakati alipompigia? Inawezekana kuna jambo alilolificha na ndilo lililomfanya mpenzi wake kumuangushia kipondo kile.

Nilipoachana na mshaoga wale, akili yangu ikazunguuka na kujiuliza hivi ni kwa nini mtu kama kweli anampenda mwenzie anafikia hatua ya kumpiga na kumumiza kiasi kile? Kweli katika mapenzi halisi, ambayo watu wanaheshimiana na kuthaminiana inawezekana kutokea kupigana?

Ili kupata majibu ya maswali haya, niliamua kuzungumza na watu kadhaa ambao nao wana mitizamo tofauti katika hili."Kiukweli katika mapenzi ya kweli na ya dhati kupigana ndio mahali pake," anasema Bi. Subira Gumbo mkazi wa Ilala Mchikichini, Bi, Gumbo anafafanua:

"Unajua saa nyingine katika mapenzi watu huwa wanatafuta 'bima' fulani ya kuhakikisha kuwa penzi lake kwa mwenzie liko salama na linaulinzi wa kutosha, kumkera mwenzio kwenye jambo ambalo unajuwa kabisa hawezi kulivumilia ni moja ya njia za kupata uhakika wa bima yako.

"Unapomtia kwenye majaribu ya wivu na ukaona kuwa amekasirika na anamua kukupiga basi hapo unapata uhakika wa bima yako kwamba penzi lako liko salama, lakini ukifanya kitu cha namna hiyo na ukaona kuwa ametulia tu, basi juwa kuwa wewe huna thamani ya mapenzi ya kweli kwake. Sie wanawake tunapenda kujaribu mambo namna hiyo, tunatafuta uhakika tu".

Inawezekana, kwamba ni kweli wanawake wengi wanaoanzisha chokochoko kwa wapenzi wao huwa wanatafuta uhakika kama kweli 'bima' yao ya mapenzi iko salama, lakini je wanaume wanalifahamu hilo? Na kama wanalifahamu wanalichukulia vipi?

"Aise linakera sana," anasema Bw. Adrean Ulaya, mkazi wa Sinza jijini Dar es Salaam na kuendelea; "unajua wanawake ingawa ni mama zetu, dada zetu na wapenzi wetu, lakini wanakera sana".

Bw. Ulaya anatoa mfano wa mke wake wa kwanza, anasimulia; "yeye alikuwa ni mwanamke mzuri na mwaminifu, lakini tatizo lake lilikuwa moja, lazima katika wiki moja atatafuta sababu mpaka nimpige, angalau kidogo tu, na nikishampiga basi siku hiyo mapenzi yake kwangu yanakuwa kama ndio yameanza leo, atakuwa mwanamke mwema kuliko unavyodhani".

Bw. Ulaya anatoa mfano wa vituko vya mke huyo ambaye bahati mbaya alifariki wakati wa uzazi kuwa; "saa nyingine alikuwa anaweza kumwaga mchele kwenye zuria au akatawanya vitu sebuleni huku akijuwa kabisa kuwa kuna wageni watakuja, ukimuuliza kwa nini anafanya hivyo atakujibu jeuri ya ajabu, na ukimpiga, hata kofi moja tu, basi atatuliana na kufanya vitu vyote kwa mpangilio wake. Ajabu kabisa!".

Ni kweli, haya ni maajabu, mtu kuchokoza ugomvi kwa makusudi, hili ni ajabu kabisa! Lakini si kwa wanawake tu wenye tabia hii ya kutaka 'kuchokoza', wapo pia wanaume wanaodaiwa kuwa na tabia hiyo ya kuchokoza lakini wao ikiwa kwa kusudi la kupiga.

"Kuna wanaume wengine bwana wakorofi," anasema Bi. Lulu Dihule, mkazi wa Kimara Temboni,  jjijini Dar es Salaam.

Bi. Dihule anatoa mfano kwa kusema; "utakuta mwanaume anarudi nyumbani kanuna, ukimuuliza mwenzangu vipi au hata kabla hujamuuliza atakuambia 'we na fulani mnajuani vipi?', utashangaa huyo fulani mwenyewe anayekuulizia labda ni mpangaji mwenzio au jirani yake, lakini akili zake za wivu tu zimemtuma akufikirie mambo mabaya na ukimjibu anakupiga".

Mikasa na visa vinavyoelezewa katika suala hili vyote vinadondokea kwenye wivu wa mapenzi, na hakuna neno zuri au tafsiri nzuri ya kuielezea kama neno alilolitumia Bi. Gumbo, kwamba wote wenye tabia hii wanatafuta uhakika wa 'bima' yao katika mapenzi, kwamba iko hai au imekufa.

Lakini, kwa Bw. Rashid Mujuni, mtabiri mchanga katika masuala ya nyota na unajimu, yeye analielezea vingine jambo hilo, anasema; "mara nyingi kupigana kwa wapenzi wanaopendana kidhati kunatokana na mchanganyiko wao kinyota".

Bw. Mujuni anafafanua; "kwa mfano watu wa nyota ya punda, hawa ni watu wakorofi katika mapenzi, ingawa kiasili ni watu wakarimu kwenye urafiki wa kawaida, na ukorofi wao katika mapenzi unatokana na tabia yao ya kupenda kupita kiasi, kwa hali hii wanatafuta sana uhakika kama wanaowapenda wanamapenzi kama ya kwao.

"Sasa inapotokea kutokuwa na uhakika na hilo, basi hugeuka na kuwa washari, wanapenda kuanzisha mambo mabaya ili waone kama kweli wapenzi wao wanawapenda kidhati, na uhakika wao kwa hilo ni kupigwa angalau kidogo tu, si mpaka uwaumize sana kwa sababu pia ni wepesi wa kubadilika na kuvutika kwa wapenzi wapya."
Inawezekana kuwa ni kwa sababu ya kutafuta uhakika wa 'bama ya penzi' au inawezekana pia ikawa kwa sababu ya athari za kinyota, lakini ukweli unabaki pale pale kuwa katika penzi la kweli kupigana kunaongeza aina fulani ya chachu ya penzi kwa sababu wale wanaopigana mara nyingi si rahisi kuachana, wana 'mapenzi sugu'.

Hata hivyo, kwa sheria zote za serikali dunia nzima, kupigana kwa aina yoyote ile ni kosa mbele ya sheria na wenye kufanya hivyo wanaweza kushitakiwa chini ya sheria hiyo.

Sunday, September 22, 2013

Katiba Mpya ilikwama tangu mwanzo


Matukio ya vurugu, kauli kinzani na hata mgawanyiko wa ndani na nje wa chama na vyama kuhusu Katiba mpya, sasa umezaa mpasuko mkubwa ambao kama hautazibwa, unaweza kuzima ndoto ya kupatikana kwa chombo hicho kabla ya mwaka 2015.
Wakati mvutano baina ya vyama vya upinzani na Serikali ya Rais Jakaya Kikwete ukishudiwa sasa kutokana na hatua ya Bunge kupitisha Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa Mwaka 2013, ndani ya vyama vya siasa nako kumeonekana kuwapo kwa mgawanyiko wa kimtazamo, hasa kuhusu kipengele cha serikali tatu, kilivyopendekezwa kwenye Rasimu ya Mabadiliko ya Katiba Mpya.

Kabla ya uelekeo wa upepo wa sasa ambao umechukua sura ya upinzani wa vyama vya upinzani (Chadema, CUF na NCCR Mageuzi) Vs Chama Cha Mapinduzi (CCM), ndani ya vyama vya CCM, Chadema na CUF tayari kulikuwa na mgawanyiko uliotokana na kuwapo kwa mitizamo tofauti kuhusu mchakato wa kupata Katiba mpya na pia kipengele hicho cha serikali tatu.

Wakati CCM na CUF wakivurugwa na kipengele cha serikali tatu, Chadema wao walikuwa wakikabiliwa na mtihani wa mwakilishi wao kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Profesa Mwesigwa Baregu, ambaye aligomea agizo la chama chake lililomtaka ajiengue katika Tume hiyo kutokana na kutoridhishwa na mchakato mzima wa kutunga Katiba mpya.

Kwa upande wa CCM, wakati Mwenyekiti wa Chama hicho, Jakaya Kikwete akiwataka wanachama wake wajiandae kisaikolojia kuhusu suala la muundo wa serikali tatu, Katibu Mkuu wake, Abdulrahman Kinana, amekuwa akisisitiza sera yao ya kuamini katika mfumo wa serikali mbili.

Vivyo hivyo kwa Chama cha Wananchi (CUF), wakati Mwenyekiti wa Chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba, akiunga mkono mfumo wa serikali tatu, licha ya kusisitiza kama ni msimamo wa pamoja wa chama, lakini zipo taarifa zinazodai kuwa baadhi ya viongozi wenzake wa upande wa Zanzibar wamekuwa wakishinikiza mfumo wa serikali ya mkataba.