Showing posts with label maisha. Show all posts
Showing posts with label maisha. Show all posts

Tuesday, September 24, 2013

Mradi wa Kigamboni kwa faida ya nani?


Wiki iliyopita niliahidi kuiendeleza hoja niliyoiandika wiki iliyotangulia kuhusiana na mradi wa ujenzi wa mji wa kisasa wa Kigamboni jijini Dar es Salaam. Kichwa cha makala ile kiliwafanya wasomaji wengi wanielewe vibaya kwa kuhoji kwa nini Kigamboni isijengwe Dodoma, wapo baadhi ya watu waliodhani kuwa ninaupinga mradi wa Kigamboni. La hasha, siupingi mradi huo hata kidogo.

Niliamua kuendelea na hoja hiyo kutokana na ujumbe mfupi wa maandishi na simu nilizopokea kutoka kwa baadhi ya wasomaji hasa mmoja ambaye alizungumza nami kwa takribani dakika 15, akijitahidi kunishawishi kuwa mradi huo ni muhimu na ni vema Serikali ikahakikisha utatekelezwa haraka. Akanihoji ni kwa nini ninaupinga?

Baada ya kunishawishi kwake nilimueleza kuwa hata mimi siupingi mradi huu, kwa sababu ni muhimu, lakini tatizo langu lipo kwenye namna unavyotekelezwa.

Baada ya kumwelewesha na kumwonyesha kwa mifano jinsi Serikali inavyokosea katika utekelezaji wa mradi huo, hatimaye tulikubaliana kuwa kuna mambo kadhaa yanayohitaji kurekebishwa ili mradi huu uwe na manufaa kwa umma na taifa kama inavyotarajiwa.

Kati ya mambo tuliyokubaliana na msomaji wangu huyo ni kuwa hadi hivi sasa, hakuna uhakika wa moja kwa moja unaoonyesha jinsi wakazi wa Kigamboni wa sasa watakavyonufaika na mradi huo.

Msomaji wangu huyo na mimi tulikubaliana kuwa pamoja na mradi kuwa na manufaa makubwa kwa taifa, lakini watu watakaoathirika na mradi huo, kama vile wakazi wa maeneo yatakayotwaliwa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi, wanapaswa kunufaika pia.

Siyo siri kuwa kwa kiasi kikubwa mradi utajengwa na wawekezaji na kila mmoja anafahamu fika kuwa ni wachache sana kati ya wawekezaji hawa, kama watakuwepo, ambao watatoka hapa nchini.

Mtu yeyote anapowekeza, lengo lake kuu la kwanza ni kupata faida kutokana na uwekezaji wake. Kwa kuwa wawekezaji hawa kutoka nje ndiyo watakaotoa fedha nyingi kwa ajili ya kuwekeza, basi na sehemu kubwa ya faida itakwenda kwao.

Serikali itabakia kupata kiasi kidogo cha kodi na ushuru (kama wawekezaji hawatapewa msamaha wa kodi).

Sasa kama Serikali yenyewe itabakia kupata fedha kidogo kupitia kodi huku sehemu kubwa ya faida ikienda kwa wawekezaji, ni nani atamtetea mwananchi mnyonge ambaye leo hii anaondolewa katika eneo lake ili kupisha mradi huo.

Kwa kuhoji kwa nini Kigamboni isijengwe Dodoma sikumaanisha kuwa mradi huo wa Kigamboni usitekelezwe Kigamboni na badala yake utekelezwe Dodoma. Nilichokuwa nafanya ni kujaribu kukumbusha kuwa ipo miradi inayofanana na hiyo, kama ule wa ujenzi wa makao makuu Dodoma, ambao umekuwa kwenye makaratasi kwa zaidi ya miaka 30 sasa, lakini hakuna dalili za utekelezaji wake.

Miradi kama hiyo imechelewa wakati haina mawaa katika utaratibu wa utekelezaji wake. Inashangaza kuwa mradi huu wa Kigamboni umebuniwa katika miaka ya hivi karibuni, lakini kasi yake ya utekelezaji inaonekana kuwa kubwa ajabu.

Tofauti baina ya miradi hii miwili ni kuwa ule wa Dodoma unapaswa kutekelezwa na Serikali, wakati huu wa Kigamboni una mkono wa wawekezaji.

Kwa umuhimu kama nchi, mradi wa Dodoma una maana kubwa kuliko huu wa Kigamboni. Lakini inashangaza kuwa Kigamboni inapewa kipaumbele zaidi ya Dodoma. Ni rahisi kuhisi hapa kuwa kuna mkono wa wawekezaji nyuma ya kasi hii ya kutaka kuwahamisha watu bila kufuata utaratibu ili lipatikane eneo la wawekezaji kutengeneza fedha zao.

Jambo jingine lianaloonyesha shinikizo la wawekezaji nyuma ya mradi huu ni jinsi Serikali ilivyoamua kuziweka kando sheria, kanuni na taratibu katika utekelezaji wa mradi wenyewe.

Mbunge wa Kigamboni, Dk. Faustine Ndugulile ameeleza vema kwenye moja ya taarifa zake.

Mbunge huyo anaeleza kuwa Wabunge wa Mkoa wa Dar es Salaam, walipokutana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, hivi karibuni ili kuujadili mradi huo pamoja na maofisa wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ilibainika kuwa sheria, kanuni na taratibu nyingi zinazohusu kubadili matumizi ya ardhi ili kuwezesha utekelezaji wa mradi huu hazikuzingatiwa na kufuatwa kikamilifu.

Ilibainika pia kuwa ushirikishwaji wa kina wa wananchi, ambao ardhi yao imepangwa kutwaliwa kwa ajili ya mradi huu haukufanyika. Wao wamekuwa wakipokea amri na maagizo kutoka ngazi za juu ambayo wanatakiwa kuyatekeleza.

Ilibainika kuwa halmashauri na Serikali za mitaa husika, ambamo eneo linalotwaliwa zimo, hawakuhusishwa.

Lakini, wizara imeenda mbali zaidi na kuunda mamlaka nyingine, Kigamboni Development Authority (KDA), ambayo itakuwa na mamlaka ya uendeshaji wa mji mpya wa Kigamboni bila kujali kuwa mamlaka hiyo imeundwa ndani ya mamlaka nyingine, Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, ambayo haikuhusishwa katika utaratibu wa uanzishwaji wa mamlaka mpya.

Mchakato huu unatawaliwa na sheria tano ikiwa ni pamoja na Sheria ya Utwaaji Ardhi namba 47 ya mwaka 1967; Sheria ya Mipango Miji namba 8 ya 2007; Sheria ya Ardhi namba 4 ya 1999; Sheria ya Wakala wa Serikali ya 1997 na Sheria ya Serikali ya Mitaa namba 8 ya 1982.

Hadi hivi sasa, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imekiuka sheria hizi katika utekelezaji wa mradi huu. Sielewi, baada ya kukiuka sheria zote hizi tano, wizara inapata wapi mamlaka ya kushinikiza mradi uendelee.

Akionyesha kutoshirikishwa kwa wananchi, Dk. Ndugulile anasema: “Watendaji wa Wizara wamekuwa hawafuati sheria na badala yake wamekuwa wakitumia ubabe, nguvu na usiri mkubwa katika utendaji kazi wao.

“Aidha, wananchi wamekuwa wakitaarifiwa na siyo kushirikishwa katika mchakato wa mradi huu. Kuna tofauti kubwa kati ya kutaarifu na kushirikisha.”

Hata kama changamoto zitatatuliwa na mradi kuendelea, katika mazingira kama hayo, hivi bado Wizara inataka tuiamini katika utekelezaji wa mradi huu?

Kama kweli kuna dhamira ya dhati, isiyo na chembe ya shinikizo kutoka upande wowote, Wizara haina budi kuhakikisha kuwa mchakato wa mradi huu unaanza upya.

Na hilo ndilo liliagizwa kwenye kikao cha Waziri Mkuu, Wabunge na maofisa wa Wizara.

Lakini, hivi ni jambo la busara kweli kuwaamini wale wale ambao walituburuta awali na kukiuka sheria, kanuni na taratibu, warudie tena kuufanya mradi huu?

Hivi tukiwaamini hawa hawa tutarajie matokeo mengine tofauti na tulichokishuhudia?

Ndiyo maana nikapendekeza katika makala yangu ya kwanza kuwa ni vema tukaelekeza nguvu kwenye mradi wa makao makuu Dodoma, ambayo itawanufaisha Watanzania moja kwa moja kuliko kujihangaisha ya Kigamboni ambayo inashinikizwa na wawekezaji kwa ajili ya faida zao.

Monday, September 23, 2013

Uvaaji wako unaathiri kinyota?


Sikuweza kuelewa kwa haraka, lakini ilinishangaza sana pale mzee mmoja wa kihindi aliponiambia; "hiyo pete yako haikufai, tafuta pete ya dhahabu na iwe na jiwe la 'saphire'".

Sikuwa namfahamu mzee huyu, nilikutana naye kwa bahati nilipokuwa kwa rafiki yangu mmoja wa kihindi mitaa ya Kariakoo, na maongezi yake yalinistusha kidogo.

Pete niliyokuwa nimevaa ni ya madini ya fedha, nimekuwa nikivaa pete hii kwa takribani miaka miwili sasa, sijawahi kuona tatizo lolote lililoletwa na pete hii, kwa hiyo kauli yake ilinishangaza na ilibidi nimuulize rafiki yangu; "huyu mzee vipi?"

Rafiki yangu alinieleza kuwa huyu mzee ni mtabiri wa nyota, kwamba kwa muda mwingi amekuwa akifanya kazi zake katika jamii ya wahindi hapa mjini na kuwa imekuwa kama bahati kwangu kukutana naye na kunieleza mambo hayo.

Huwa siamini masuala ya nyota, lakini kwa muda mchache uliofuata baada ya mazungumzo na mzee huyo wa kihindi nilianza kuhisi kama naanza kubadilika kimawazo, nikaanza kuamini kidogo masuala hayo.
Kwa tarehe yangu ya kuzaliwa na mwezi, Novemba 24, mzee yule aliniambia kuwa nyota yangu ni mshale, hilo halikunishangaza kwa sababu nalijua siku nyingi, lakini alichonieleza ambacho sikuwa nakijua, ni mambo mengine ya watu wa nyota hiyo.

Alinieleza mambo mengi ya watu wa 'mshale', ambayo kwa hakika mengi yalikuwa yanafanana na mambo yangu binafsi, akanieleza na tabia za watu wa nyota yangu, ambayo nayo yalikuwa karibu sawa na tabia zangu.

"Wewe una tabia ya kuwa na matumaini kuwa utafanikiwa kwa jambo lolote unalofanya au unalotegemea kupata," alisema mzee huyo na kuendelea; "unapenda kuwa na uhuru wa kufanya mambo yako hata kama watu watakuambia kuwa jambo hilo ni baya na unapenda watu wengine wawe kama wewe".

Mzee huyu aliendelea kunieleza kuwa mimi ni mtu nisiyependa kuamrishwa kufanya jambo kwa sababu naamini kuwa nina uwezo mkubwa wa kufanya jambo lolote; "na ukiudhiwa unakuwa mkaidi na hutii amri ya mtu yoyote", alisema.

Kwa mujubu wa elimu yake, mzee huyu alisema; "hali hiyo inasababishwa na mtawala wa nyota yako, ambayo ni moto, moto ni kitu kizuri kwa watu, lakini watu wanapoutumia vibaya moto huwa na madhara kwao, lazima utaleta hasara."

Kwa muda mzee huyu aliendelea 'kunichambu' kwa jambo moja baada ya jingine, akasema; "katika mapenzi, kwa nyota yako wewe ni mtu ambaye unapoanzisha uhusiano unakuwa ni mwaaminifu, lakini kinyota unapenda kila wakati kuwa na wapenzi wapya au mapenzi ya kawaida, sio ya kudumu, kwa sababu unaona mapenzi ya kudumu yakunyima uhuru."

Kwa kuona hali yangu ya kushitushwa na mazungumzo hayo, mzee huyu wa kihindi ambaye mida wote alikuwa akitabasamu, aliwahi haraka kunieleza kuwa; "hii ni nyota tu baba, unaweza kujibadili ukipenda".

Inawezekana kuwa na wewe ni mtu wa nyota ya mshale kama mimi, ikiwa hivyo unaweza kuchukuwa maneno ya mzee huyu kama changamoto kwako na kujichunguza kitabia kuona kama yanaendana na wewe.

Kwa upande wa kazi, mzee huyu alisema; "kwa nyota yako wewe unatakiwa kufanya kazi za kusafiri safiri hivi, kazi za sheria; uwakili au uhakimu, kazi za uandishi, ualimu, kazi za kidini; uwe sheikh au padri au kazi zozote za makanisani au misikitini, kazi za michezo, kazi za kijeshi na biashara hasa ya kuuza vitu."

Pia hakuacha kunichagulia mavazi, alisema; "kwa nyota yako wewe unatakiwa kuvaa mavazi ya
nguo zenye zambarau au rangi ya kahawia iliyochangamka au rangi ya blue na ziwe za vitambaa vya sufu na zimeshona kiutamaduni kwa kuchanganya rangi au ukivaa koti na suruali basi zisiwe katika mpangilio wa rangi moja, ziwe za kuchekesha chekesha hivi".

Niliuliza; "kwa wanawake wa nyota hii nao je, wanatakiwa wavae mavazi gani?" nikajibiwa kuwa sketi na blauzi ni mavazi mazuri kwao na rangi zao ziwe hizo na siku za nzuri kwa watu wote wa mshale ni Alhamisi na namba yao ya bahati ni namba tatu.

Baada ya kupata utabiri huo, wa bure, nilishawishia kutaka kujuwa kama kuna watu wengine wanaovaa nguo au vito huku wakijua ni nini athari au maana ya kuvaa vito hivyo? Utafiti wangu nilifanya zaidi kwa watu ambao walikuwa wamevaa pete zenye vitu maalumu.

Mzee Sadiq Izunya, mkazi wa Kariakoo, yeye anavaa pete yenye kito cha marijani, anasema; "ni kweli pete hizi tunazivaa kwa maana, mimi nilikuwa na maradhi mabaya ya nyonga, nimejaribu kutibiwa sehemu mbalimbali lakini sikupa nafuu, ila bwana mmoja 'mtaalamu' alinishauri nivae pete hii na kutumia dawa nikapona."

Kama mzee Izunya, watu wengi niliowakuta na pete zenye vito walizieleza pete hizo kuwa zina maana maalum, wengi wao wakiwa wamevaa kwa ushauri wa waganga au wengine kwa imani ya masuala ya nyota.

Katika utafiti huo mdogo, niligundua pia wapo watu ambao huamua kuweka vito hivyo baada ya kushauriwa na masonara ambao wao huwa na orodha ya aina za vito kwa mujibu wa nyota za watu.

Katika hali hiyo, ya kufuata nyota kwa vito kwa kuzingatia alama zake, inashauriwa na wataalam wa masuala hayo mtu asipende kuvaa kito bila ya kujua maana yake au nini madhara ya kito hicho kwa upande wa nyota yake, lakini inawezekana pia kuwa jambo hilo ni sahihi au si sahihi.