Thursday, November 21, 2013

Dally estate images




Dally estate images



Wednesday, September 25, 2013

Wadau wamtabiria makubwa Miss Tanzania


Ni Happiness Watimanywa, alitangazwa juzi kuwa mshindi wa taji hilo baada ya safari ndefu ya kuanzia ngazi ya vitongoji, m
koa na kanda.

Dar es Salaam. Juzi katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam, kamati ya shindano kubwa la urembo lenye sura ya Kitaifa, linalojulikana kwa jina la Redd’s Miss Tanzania 2013, lilimtawaza Happiness Watimanywa kuwa mshindi wa taji hilo baada ya safari ndefu ya kuanzia ngazi ya vitongoji, mkoa, na kanda.

Wadau wengi wa masuala ya urembo wanamtabiri Happiness Watimanywa kwamba huenda ataifikisha mbali Tanzania katika medani ya urembo kutokana na uelewa wake na jinsi anavyoweza kujieleza kwa ufasaha, pia kutokana na upeo alionao katika masuala ya kimataifa.

Katika mahojiano na gazeti hili baada ya shindano hilo, wadau mbalimbali wa burudani wameonyesha imani na msichana huyo anayeonekana kuwa na umri mdogo lakini mwenye upeo wa hali ya juu.

Sospeter Gerald, mbunifu wa mavazi na mtaalamu wa urembo kutoka Kenya ambaye amekuwa akifuatilia historia ya Tanzania katika masuala ya urembo kwa muda mrefu ameliambia gazeti hili kwamba safari hii, wanaweza kufika mbali kutokana na mwakilishi wao kuonekana kuwa na uwezo katika kujieleza na mwonekano pia.

Naye Alice Mutalemwa, ambaye ni mwanamitindo, aliliambia gazeti hili  kwamba Hapinness, anahitaji tu kukaa na dada mwenye hekima, amwelekeze njia, kutokana na umri wake na majaribu yaliyomo kwenye tasnia, lakini kwa jinsi alivyoonekana, anaweza kufika mbali.

Kumbukumbu za masuala ya elimu ya kimataifa zinamkumbuka binti huyo mwenye umri wa miaka 19, ni mzaliwa wa familia ya Louis Roussos ya Morogoro, amewahi kusoma Laureatte International School ya Dar es Salaam, ambapo akiwa hapo, aliwahi kwenda China na Korea kusini akiwa na wanafunzi wenzake katika matamasha mbalimbali ya elimu na michezo.

Baada ya kumaliza kidato cha nne, Happy alifanikiwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Strathclyde cha Uingereza anasomea digrii ya Biashara.Kipindi ambacho Happy yupo kwenye likizo ndefu, alipata wakati mgumu wa kutokuwa na kitu cha kufanya, hivyo Happy aliamua kujihusisha na masuala ya urembo na kufanikiwa kutwaa Taji la Miss Dodoma na Miss Kanda ya Kati na hatimaye kuingia kwenye kambi ya Miss Tanzania.

Tuesday, September 24, 2013

Mradi wa Kigamboni kwa faida ya nani?


Wiki iliyopita niliahidi kuiendeleza hoja niliyoiandika wiki iliyotangulia kuhusiana na mradi wa ujenzi wa mji wa kisasa wa Kigamboni jijini Dar es Salaam. Kichwa cha makala ile kiliwafanya wasomaji wengi wanielewe vibaya kwa kuhoji kwa nini Kigamboni isijengwe Dodoma, wapo baadhi ya watu waliodhani kuwa ninaupinga mradi wa Kigamboni. La hasha, siupingi mradi huo hata kidogo.

Niliamua kuendelea na hoja hiyo kutokana na ujumbe mfupi wa maandishi na simu nilizopokea kutoka kwa baadhi ya wasomaji hasa mmoja ambaye alizungumza nami kwa takribani dakika 15, akijitahidi kunishawishi kuwa mradi huo ni muhimu na ni vema Serikali ikahakikisha utatekelezwa haraka. Akanihoji ni kwa nini ninaupinga?

Baada ya kunishawishi kwake nilimueleza kuwa hata mimi siupingi mradi huu, kwa sababu ni muhimu, lakini tatizo langu lipo kwenye namna unavyotekelezwa.

Baada ya kumwelewesha na kumwonyesha kwa mifano jinsi Serikali inavyokosea katika utekelezaji wa mradi huo, hatimaye tulikubaliana kuwa kuna mambo kadhaa yanayohitaji kurekebishwa ili mradi huu uwe na manufaa kwa umma na taifa kama inavyotarajiwa.

Kati ya mambo tuliyokubaliana na msomaji wangu huyo ni kuwa hadi hivi sasa, hakuna uhakika wa moja kwa moja unaoonyesha jinsi wakazi wa Kigamboni wa sasa watakavyonufaika na mradi huo.

Msomaji wangu huyo na mimi tulikubaliana kuwa pamoja na mradi kuwa na manufaa makubwa kwa taifa, lakini watu watakaoathirika na mradi huo, kama vile wakazi wa maeneo yatakayotwaliwa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi, wanapaswa kunufaika pia.

Siyo siri kuwa kwa kiasi kikubwa mradi utajengwa na wawekezaji na kila mmoja anafahamu fika kuwa ni wachache sana kati ya wawekezaji hawa, kama watakuwepo, ambao watatoka hapa nchini.

Mtu yeyote anapowekeza, lengo lake kuu la kwanza ni kupata faida kutokana na uwekezaji wake. Kwa kuwa wawekezaji hawa kutoka nje ndiyo watakaotoa fedha nyingi kwa ajili ya kuwekeza, basi na sehemu kubwa ya faida itakwenda kwao.

Serikali itabakia kupata kiasi kidogo cha kodi na ushuru (kama wawekezaji hawatapewa msamaha wa kodi).

Sasa kama Serikali yenyewe itabakia kupata fedha kidogo kupitia kodi huku sehemu kubwa ya faida ikienda kwa wawekezaji, ni nani atamtetea mwananchi mnyonge ambaye leo hii anaondolewa katika eneo lake ili kupisha mradi huo.

Kwa kuhoji kwa nini Kigamboni isijengwe Dodoma sikumaanisha kuwa mradi huo wa Kigamboni usitekelezwe Kigamboni na badala yake utekelezwe Dodoma. Nilichokuwa nafanya ni kujaribu kukumbusha kuwa ipo miradi inayofanana na hiyo, kama ule wa ujenzi wa makao makuu Dodoma, ambao umekuwa kwenye makaratasi kwa zaidi ya miaka 30 sasa, lakini hakuna dalili za utekelezaji wake.

Miradi kama hiyo imechelewa wakati haina mawaa katika utaratibu wa utekelezaji wake. Inashangaza kuwa mradi huu wa Kigamboni umebuniwa katika miaka ya hivi karibuni, lakini kasi yake ya utekelezaji inaonekana kuwa kubwa ajabu.

Tofauti baina ya miradi hii miwili ni kuwa ule wa Dodoma unapaswa kutekelezwa na Serikali, wakati huu wa Kigamboni una mkono wa wawekezaji.

Kwa umuhimu kama nchi, mradi wa Dodoma una maana kubwa kuliko huu wa Kigamboni. Lakini inashangaza kuwa Kigamboni inapewa kipaumbele zaidi ya Dodoma. Ni rahisi kuhisi hapa kuwa kuna mkono wa wawekezaji nyuma ya kasi hii ya kutaka kuwahamisha watu bila kufuata utaratibu ili lipatikane eneo la wawekezaji kutengeneza fedha zao.

Jambo jingine lianaloonyesha shinikizo la wawekezaji nyuma ya mradi huu ni jinsi Serikali ilivyoamua kuziweka kando sheria, kanuni na taratibu katika utekelezaji wa mradi wenyewe.

Mbunge wa Kigamboni, Dk. Faustine Ndugulile ameeleza vema kwenye moja ya taarifa zake.

Mbunge huyo anaeleza kuwa Wabunge wa Mkoa wa Dar es Salaam, walipokutana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, hivi karibuni ili kuujadili mradi huo pamoja na maofisa wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ilibainika kuwa sheria, kanuni na taratibu nyingi zinazohusu kubadili matumizi ya ardhi ili kuwezesha utekelezaji wa mradi huu hazikuzingatiwa na kufuatwa kikamilifu.

Ilibainika pia kuwa ushirikishwaji wa kina wa wananchi, ambao ardhi yao imepangwa kutwaliwa kwa ajili ya mradi huu haukufanyika. Wao wamekuwa wakipokea amri na maagizo kutoka ngazi za juu ambayo wanatakiwa kuyatekeleza.

Ilibainika kuwa halmashauri na Serikali za mitaa husika, ambamo eneo linalotwaliwa zimo, hawakuhusishwa.

Lakini, wizara imeenda mbali zaidi na kuunda mamlaka nyingine, Kigamboni Development Authority (KDA), ambayo itakuwa na mamlaka ya uendeshaji wa mji mpya wa Kigamboni bila kujali kuwa mamlaka hiyo imeundwa ndani ya mamlaka nyingine, Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, ambayo haikuhusishwa katika utaratibu wa uanzishwaji wa mamlaka mpya.

Mchakato huu unatawaliwa na sheria tano ikiwa ni pamoja na Sheria ya Utwaaji Ardhi namba 47 ya mwaka 1967; Sheria ya Mipango Miji namba 8 ya 2007; Sheria ya Ardhi namba 4 ya 1999; Sheria ya Wakala wa Serikali ya 1997 na Sheria ya Serikali ya Mitaa namba 8 ya 1982.

Hadi hivi sasa, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imekiuka sheria hizi katika utekelezaji wa mradi huu. Sielewi, baada ya kukiuka sheria zote hizi tano, wizara inapata wapi mamlaka ya kushinikiza mradi uendelee.

Akionyesha kutoshirikishwa kwa wananchi, Dk. Ndugulile anasema: “Watendaji wa Wizara wamekuwa hawafuati sheria na badala yake wamekuwa wakitumia ubabe, nguvu na usiri mkubwa katika utendaji kazi wao.

“Aidha, wananchi wamekuwa wakitaarifiwa na siyo kushirikishwa katika mchakato wa mradi huu. Kuna tofauti kubwa kati ya kutaarifu na kushirikisha.”

Hata kama changamoto zitatatuliwa na mradi kuendelea, katika mazingira kama hayo, hivi bado Wizara inataka tuiamini katika utekelezaji wa mradi huu?

Kama kweli kuna dhamira ya dhati, isiyo na chembe ya shinikizo kutoka upande wowote, Wizara haina budi kuhakikisha kuwa mchakato wa mradi huu unaanza upya.

Na hilo ndilo liliagizwa kwenye kikao cha Waziri Mkuu, Wabunge na maofisa wa Wizara.

Lakini, hivi ni jambo la busara kweli kuwaamini wale wale ambao walituburuta awali na kukiuka sheria, kanuni na taratibu, warudie tena kuufanya mradi huu?

Hivi tukiwaamini hawa hawa tutarajie matokeo mengine tofauti na tulichokishuhudia?

Ndiyo maana nikapendekeza katika makala yangu ya kwanza kuwa ni vema tukaelekeza nguvu kwenye mradi wa makao makuu Dodoma, ambayo itawanufaisha Watanzania moja kwa moja kuliko kujihangaisha ya Kigamboni ambayo inashinikizwa na wawekezaji kwa ajili ya faida zao.

Azam TV itakavyohatarisha utawala Simba na Yanga


Kabla ya Ligi Kuu ya Vodacom haijaanza, Kamati ya
Ligi ilikuwa kwenye mchakato wa kutafuta mdhamini wa kuonesha moja kwa moja ‘live’ Ligi hiyo, ambapo Kampuni za Multichoice kupitia Kituo chake cha Supersports na Kampuni ya Azam Media kupitia Azam TV, walijitokeza kutaka kupewa nafasi ya kumiliki haki za matangazo hayo ya ligi.

Azam Media ambayo ndiyo imeanzishwa mwaka huu, ilishinda katika mchakato huo na kufanikiwa kupata haki za kuonesha ‘live’ ligi hiyo, ambapo walisaini mkataba wa kudhamini ligi kwa misimu mitatu ijayo wakianza na msimu huu.

Mkataba uliogharimu Sh bilioni 5.6 kwa misimu yote ya udhamini huo.

Mpaka sasa klabu 13 za ligi hiyo, zimeshapokea sehemu ya fedha za awali kutoka Azam TV kwa ajili ya udhamini wa msimu huu, ambapo kila timu imepewa milioni 25, huku zikibakia milioni 75 ambazo watapewa miezi miwili ijayo, kwani kwenye msimu huu kila timu zitapokea Sh milioni 100.

Klabu ya Yanga bado haijapewa fedha hizo, baada ya klabu hiyo kupinga udhamini huo, wakidai itawafanya mashabiki wao kutokwenda kwa wingi uwanjani katika mechi zao, kwani wanategemea kwa kiasi kikubwa fedha za milangoni kwenye uendeshaji wa klabu.

Hivi sasa wapo kwenye mazungumzo na kampuni hiyo kufanya makubaliano mengine nje ya udhamini huo, ambayo yatawaingizia fedha za ziada.

Msimu uliopita, klabu za ligi hiyo zilitaka kumgomea mdhamini wa ligi, Kampuni ya Vodacom kutokana na kipengele cha kutoruhusu mpinzani wake (kampuni nyingine ya mawasiliano ya simu za mkononi), kuingia udhamini na klabu hizo, lakini baadaye walikubali kucheza wakiheshimu sheria za soka na pia mkataba wa kampuni hiyo.

Ligi hiyo imefikia raundi ya tano hivi sasa, ambapo tumeshuhudia upinzani mkali unaooneshwa na timu zote, hasa baada ya kuchagizwa na udhamini mnono wanaoupata kwa wadhamini wa Ligi hiyo, Vodacom na Azam TV.

Klabu zote zimefanya usajili mzuri na pia udhamini umewasaidia kuziandaa vyema timu zao na hawana matatizo mengi ya kifedha kama yaliyokuwa kipindi cha nyuma wakati ligi ikiwa na mdhamini mmoja pekee.

Klabu kongwe za Simba na Yanga, zilikuwa zinatawala soka nchini kwa kuzionea timu ndogo kila msimu, lakini msimu huu hali ni tofauti, kwani timu hizo zimecheza mechi mbili viwanja vya mikoani, Simba imeambulia pointi nne pekee kati ya sita huku ya Yanga ikiambulia pointi mbili pekee.

Hata kauli za makocha na viongozi wa timu hizo, wamekiri msimu huu si mchekea kama ilivyo kipindi cha nyuma, wakisema wamekuwa wakikamiwa sana na timu mbalimbali wanazocheza nazo kwenye mechi za ligi, hasa wakihofia viwanja vya mikoani.

Kocha Juma Mwambusi anayeifundisha timu ngumu ya Mbeya City, amefanikiwa kuzikaba koo timu hizo katika mechi alizokutana nao, akiibana Yanga kwa sare ya 1-1 na pia Simba kwa sare ya 2-2, huku Simba ikiwa mbele ya mashabiki wake waliojazana katika Uwanja wa Taifa.

Pia hata klabu nyingine za Azam na Coastal Union ambazo zina wachezaji wa gharama kubwa, nazo zimekuwa zikionja ugumu wa ligi hiyo, ambayo imefikia robo ya msimu hivi sasa.

Ukiangalia kwenye msimamo wa ligi mpaka hivi sasa, utagundua ugumu ninaouzungumzia hapa, kwani ukianzia kwa Simba inayoongoza Ligi hiyo, timu zimepishana pointi mbili kimsimamo na timu yoyote inayoshinda mchezo wake hujikuta imepanda sana kwenye msimamo.

Hali hii ndiyo ilikuwa inatafutwa kwa muda mrefu katika mapinduzi ya soka letu na kwa hakika utawala wa Simba na Yanga utapotea kadiri misimu itakavyokuwa ikienda mbele.

Kwani muda mfupi ujao tutashuhudia timu zikipata udhamini mwingine binafsi na ule wa wadhamini wa ligi, ambao utaongeza ugumu zaidi ya huu tunaoushuhudia hivi sasa.

Klabu ya Ashanti United imeshaanza kuneemeka mapema, hasa baada ya Kampuni ya Bakhresa, kuwapa udhamini wenye thamani ya Sh milioni 35 kwa ajili ya msimu huu.

Kwa hakika mapinduzi yameanza kuonekana na kikubwa ni fahari kwa nchi yetu, kwani itachochea maendeleo ya mchezo huu na kufikia kule wenzetu walipoendelea na yote hayo yamesababisha na timu zote kujiweza kifedha kupitia udhamini walioupata.

Mtunisi: Wasanii waache ubaguzi


Msanii wa filamu nchini, Nice Mohamed ‘Mtunisi’, amesema baadhi ya wasanii wa filamu nchini, wana tabia ya kubagua wenzao katika kila shughuli zinazohitaji umoja wao.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii, Mtunisi alisema tabia hiyo itajenga chuki na kupunguza idadi ya wasanii kuhudhuria vikao na shughuli zinazohitaji umoja wao ili zifanikiwe.

“Siku hizi hakuna upendo wala ushirikiano kati yetu wasanii, wengi wana ubinafsi na hawajali wenzao, kwa mtindo huu hatuwezi kufikia mafanikio. Inatupasa tushirikiane kwa upendo wa kweli na si unafiki,’’ alisema Mtunisi.

Chidumule aukosoa muziki wa dansi


Mwanamuziki mkongwe nchini, Cosmas Chidumule, amesema muziki wa dansi hauna nidhamu na ndiyo maana ameamua kuachana nao baada ya kuokoka ili amrudie Mungu.

Chidumule aliyasema hayo hivi karibuni, jijini Dar es Salaam, kuwa mara nyingi wanamuziki wa dansi na wengineo thamani yao inakuwa ndogo mbele ya hadhira.

Alisema wengineo hufika mbali kwa kuamua kuwatuza waimbaji bangi au vitu vingine visivyokuwa na manufaa katika maisha yao, jambo ambalo ameamua kuachana nalo.

“Huu ni wakati wa kumrudia Mungu, maana si mara zote waimbaji wanakuwa na thamani kwa mashabiki wao na ndiyo maana baadhi yao wanatunzwa bangi,” alisema.